Mjumbe maalumu wa Libya kwenye Umoja wa Mataifa Ghassan Salame amesema Libya inatakiwa kuanza mchakato wa kisiasa mapema mwaka ujao. Ameliambia baraza la usalama la Umoja wa Mataifa kuwa viongozi wanne wanaokinzana kwenye taifa hilo lililoharibiwa na vita walikubaliana mapema mwaka huu kufanya vikao vya bunge na chaguzi za urais ifikapo Disemba 10, ingawa yamekuwa yakiahirishwa na kukabiliwa na mivutano katika miezi kadhaa baada ya maafikiano, ambayo kulingana na mjumbe huyo yalilenga kupoteza muda. Salame ametaka kuitishwa kwa kongamano la kitaifa katika wiki za mwanzo wa mwaka 2019, na kufuatiwa na kuanza kwa mchakato wa uchaguzi wakati wa majira ya machipuko. Alirejelea uchunguzi wa maoni ulioonyesha asilimia 80 ya raia wa Libya wanasisitiza kufanyika kwa chaguzi. Libya iliingia kwenye mgogoro tangu kulipuka machafuko ya mwaka 2011, na hatimaye kuondolewa madarakani aliyekuwa kiongozi wa taifa hilo Muammar Gaddafi.