Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan, ameridhia kibali cha kuajiri watumishi Elfu 21 na mia 2 wa Kada za Ualimu na Afya.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma leo Aprili 12, 2023 Waziri wa TAMISEMI Mhe Angellah Kairuki, amesema kuwa Idadi ya Watumishi watakaoajiriwa katika Kada za Ualimu ni Elfu 13 mia 1 na 30 ambao watafundisha katika shule za Msingi na Sekondari.
Aidha idadi ya watumishi watakaoajiriwa katika kada za Afya ni Elfu 8 na 70 ambao watafanya kazi katika Hospitali za Halmashauri, Vituo vya Afya na Zahanati.
Aidha Mhe Kairuki amesema waombaji wote wanatakiwa kuwa wahitimu wa mwaka 2015 mpaka 2022 kutoka katika vyuo vya elimu ya juu na vya kati kwenye fani ya Ualimu na Afya vinavyotambuliwa na Serikali.
Mhe Kairuki amesema waombaji wanatakiwa kuomba ajira kuanzia leo April 12 hadi 25 2023 saa 5:59 usiku.