Wakati wiki ya sheria inaendelea katika maeneo mbalimbali hapa nchini, wakazi wameshauriwa kujitokeza kwa wingi kwenda katika viwanja vya nyerere square kwaajili ya kupata elimu zaidi Kuhusiana na masuala ya kisheria kwani muamko wa watu umeonekana kuwa ni mdogo.
Akizingumza uwanjani hapo, Afisa Uchunguzi kutoka Idara ya Sheria wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora Bwana, Fadhili Muganyizi amesema kuwa muamko umekuwa mdogo ukilinganishwa na vipindi vingine vilivyopita.
Mbali na Masuala mengine,amesema taasisi yao imekuwa ikipokea malalamiko ambayo yanahusiana na masuala uvunjifu wa haki binadamu na utawala bora na kushughulikiwa kikamilifu.
Ameongeza kuwa katika kuwafikia wananchi walioko vijijini kutokana na changamoto ambazo wamekuwa wakizipata hasa kuhusiana na matatizo ya haki za binadamu wamekuwa wakifanya ziara kwa wananchi kwaajili ya wao kuweza kuifanya kazi kubwa ambayo imekuwa ikifanywa na Tume.
Kwa upande wake Said Rashid ambaye ni Afisa Uchunguzi wa Tume hiyo amesisitiza watu kujitokeza kwa wingi katika maonesho maadhimisho ya wiki ya sheria yanayoendelea katika viwanja hivyo kwani muamko hauridhishi.
Ikumbukwe kuwa Maadhimisho ya wiki ya sheria Jijini Dodoma yalizinduliwa kitaifa na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh John Ndugai alilisitiza wananchi kujitokeza katika wiki ya sheria kwaajili ya kupata elimu juu ya masuala ya kisheria.
Maadhimisho haya yanakwenda sambamba na kauli mbiu isemayo ‘’Uwekezaji na Biashara;Wajibu wa Mahakama na Wadau kuweka Mazingira Wezeshi ya uwekezaji.


