Jeshi la Kujenga Taifa [JKT] limewataka vijana wote waliohitimu kidato cha sita mwaka 2026 kutoka shule zote za Tanzania Bara na Visiwani kuhudhuria mafunzo ya JKT kundi la lazima.
Akitoa taarifa jijini Dodoma kwa niaba ya Mkuu wa JKT Meja Jenerali Rajabu Mabele, Mkuu wa Tawi la Utawala Brigedia Jenerali Hasani Mabena alisema vijana hao wamepangiwa makambi mbalimbali nchini na wanatakiwa kuripoti kuanzia tarehe 1 hadi 7 Juni 2026.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, wahitimu wenye ulemavu wa kimwili wametakiwa kuripoti katika Kambi ya Ruvu iliyopo Mlandizi, mkoani Pwani, kutokana na kuwa na miundombinu inayozingatia mahitaji yao.
JKT imesema orodha kamili ya majina ya vijana waliochaguliwa, makambi waliyopangiwa na vifaa vinavyotakiwa inapatikana kwenye tovuti rasmi ya JKT. Ili kujua kambi aliyopangiwa, mhitimu atatakiwa kuingiza jina au namba ya shule aliyohitimu kidato cha sita, kisha kuchagua chaguo la “waliochaguliwa” ili kuona taarifa kamili.
Vilevile, mtumiaji anaweza kupakua faili la PDF 2026 lililowekwa juu kulia kwenye ukurasa huo kwa ajili ya kuona majina na makambi yote.
Meja Jenerali Mabele amewakaribisha vijana wote waliohitimu kujiunga na wenzao ili kujengewa uzalendo, nidhamu, ukakamavu, umoja wa kitaifa, stadi za kazi na maisha, pamoja na utayari wa kulijenga na kulitumikia Taifa.



