Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, amemuasili leo mtoto mchanga wa kike aliyepewa jina Grace Samia Suluhu, katika makazi yake, Ikulu Chamwino, mkoani Dodoma.
Mtoto huyo alitelekezwa mjini Nzega, mkoani Tabora, na amekabidhiwa kwa Rais Dkt. Samia na Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Mhe. Naitapwaki Tukai. Akizungumza wakati wa kumkabidhi, Mkuu wa Wilaya Tukai alieleza kuwa mtoto huyo aliokotwa tarehe 17 Januari 2026 karibu na nyumba ya wageni ya Kasulu, Nzega Mjini.
“Tarehe tuliopokea taarifa, tulishirikiana na Jeshi la Polisi kumchukua mtoto na kumpeleka hospitalini kwa uchunguzi na uangalizi maalum. Juhudi za kumtafuta mama yake zinaendelea bila mafanikio hadi sasa,” alisema Mkuu wa Wilaya.
Rais Dkt. Samia amemkaribisha mtoto huyo katika familia yake na kuahidi kumpatia malezi, ulinzi wa kisheria, na huduma zote muhimu za msingi, kuhakikisha akue katika mazingira salama, yenye upendo na maendeleo stahiki.
Rais Dkt. Samia pia alisisitiza umuhimu wa kutoa watoto waliotelekezwa kwa mamlaka husika
“Wanaotupa watoto hawajui wanalolifanya. Kuliko kumtupa mtoto ni bora kumkabidhi katika mamlaka za kisheria au kituo cha kulelea watoto. Kila mtoto aliyezaliwa ni hazina, na hatuwezi kujua kesho yake.”
Uamuzi huu unaashiria dhana ya Serikali ya kulinda haki za watoto, kuhakikisha usalama wao, na kutoa malezi bora kwa watoto wote walio hatarini.
#radio5fm



