SERIKALI imekiri kwamba wingi wa ushuru wa mazao wanaotozwa wakulima ni kikwazo kimojawapo katika kuwakomboa wakulima hivyo imeamua kupunguza asilimia 50 ya ushuru katika bajeti ya mwaka ujao wa fedha ya 2017/18.
Imesema pia kuwa imeandaa mpango maalumu wa kuhakikisha kuwa kufikia msimu wa 2018/2019 wakulima wa pamba kote nchini wanatumia mbegu bora aina ya UKM08 zenye tija kubwa badala ya mbegu aina ya UK91 ,ambayo imepoteza ubora wake.
Hayo yamesemwa bungeni na Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, William ole Nasha alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Bunda, Boniface Geter (CCM) na swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalumu, Munde Tambwe (CCM).
Katika swali la msingi, Gatere alitaka kujua mkakati wa serikali wa kuwapatia zao mbadala wakulima wa pamba, baada ya zao hilo kuelekea kutokomea kutokana na matatizo ya bei ndogo isiyokidhi mahitaji ya uzalishaji wake.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri alisema serikali inakiri kuwepo kwa changamoto ya tozo nyingi ambayo ni changamoto kwa wakulima. Naibu Waziri alisema wizara kwa kuona umuhimu wa jambo hilo imeamua kupunguza zaidi ya nusu ya tozo.
Kuhusu zao la pamba amesema, serikali imeendelea kusimamia upatikanaji viuatilifu bora, na matumizi sahihi ili kuhakikisha wakulima wanatumia na kupata pamba iliyo na ubora .
