Tanzania na Singapore ni marafiki wa muda mrefu na mwaka huu wanasherehekea miaka 45 ya uhusiano wa kidiplomasia.
Uhusiano huu si wa kihistoria pekee, bali pia umejikita katika ushirikiano wa kiuchumi na maendeleo ya kijamii.
Kwa sasa, Singapore imewekeza miradi 36 nchini Tanzania yenye thamani ya Dola milioni 535.13 za Marekani na imezalisha ajira 3,228 kwa Watanzania. Sekta zinazoguswa ni kilimo, usafirishaji, ujenzi, na rasilimali za asili.

Ziara ya siku tatu ya Rais wa Singapore, Tharman Shanmugaratnam, kwa mwaliko wa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, inalenga kuimarisha zaidi maeneo ya ushirikiano.
Wakuu hao watajadili biashara na uwekezaji, maendeleo ya bandari na usafirishaji, uchumi wa kidijitali, elimu na mafunzo ya ujuzi, utalii, miundombinu, teknolojia na ubunifu, pamoja na maendeleo endelevu.
Uhusiano huu unatarajiwa kuendelea kuimarika, na kuleta fursa zaidi za uwekezaji, ajira, na maendeleo ya miundombinu. Kwa Watanzania, hii ni nafasi ya kushiriki katika uchumi wa kidijitali na kujiweka katika ramani ya kimataifa.



