Rais wa ukraine Volodymyr Zelensky ameonya jana kwamba Urusi inajiandaa kuongeza mashambulizi wiki hii wakati taifa hilo likisubiri uamuzi wa kihistoria wa Umoja wa Ulaya juu ya ombi la kujiunga na umoja huo. Zelensky hata hivyo amesema wanajiandaa na wako tayari na hatua hiyo ya Urusi. Amesema hayo siku moja baada ya ziara ya nadra nje ya mji wa Kyiv ambako alikutana na kuwasalimia wanajeshi kwa mara ya kwanza tangu Urusi ilipolivamia taifa hilo. Amesema katika video aliyoirusha kwenye mtandao wa Telegram wakati akirejea Kyiv ya kwamba kamwe hawatamuachia yoyote eneo la kusini na kuahidi kurejesha kila kilichochukuliwa. Katibu mkuu wa Jumuiya ya Kujihami ya NATO Jens Stoltenberg tayari ameonya kwamba vita hivyo vitadumu kwa muda mrefu na kuyaomba mataifa ya magharibi kujiandaa kutoa misaada ya muda mrefu ya kijeshi, kisiasa na ya kiuchumi.