Wadau wa Mfuko wa Afya wa pamoja nchini (Health Basket
Fund) wamepanga kuchangia kiasi cha shilingi Bilioni 98.1 kwa
ajili ya kuboresha utoaji wa huduma za afya nchini kwa mwaka
2022/2023.
Hayo ya mesemwa na Waziri wa afya Mhe. Ummy Mwalimu
wakati wa kikao cha kujadili uboreshaji wa mfuko huo kupitia
ushirikiano wa pamoja kati ya Serikali na wadau Jijini Dar Es
Salaam.
Waziri Ummy amesema katika mwaka wa fedha uliopita wadau
kupitia Mfuko walichangia kiasi cha shilingi bilioni 74.3
ambapo asilimia 90 ya fedha zimekwenda kwenye Halmashauri
na zimeingizwa moja kwa moja kwenye Zahanati, Vituo vya
Afya pamoja na Hospitali za Wilaya nchini.
Aidha, Waziri Ummy Mwalimu amesema upo umuhimu kwa
wadau wa maendeleo kuchanga fedha kwa pamoja na kuweka
kwenye Mfuko wa Afya wa pamoja na kusema kuwa kufanya
hivyo ni kuzingatia Mifumo na taratibu za Serikali za kutoa
fedha kwa ajili ya Huduma za Afya nchini pamoja na kuwekeza
fedha kwenye maeneo ya vipaumbele vya Serikali.
Kwa upande wake Naibu Waziri kutoka Ofisi ya Rais
TAMISEMI Mheshimiwa Dkt. Festo Dugange ameshukuru
wadau hao kwa kuendela kutoa ushirikiano na Serikali na kutoa
fedha kwa ajili ya kuboresha utoaji wa huduma katika vituo vya
kutolea huduma za afya nchini.
akizungumza na vyombo vya Habari Dkt. Peter Nyela Meneja
wa Program ya Afya kutoka Ubalozi wa Ireland kwa niaba ya
Wadau wanaochangia katika Mfuko wa Afya wa
pamoja,amesema wanafanya hivyo kusaidia Serikali ili
kuhakikisha Vituo vya kutolea huduma za afya nchini vinakuwa
na dawa, kurahisisha huduma nyinginezo ikiwemo huduma za
rufaa, pamoja na motisha kwa watoa huduma za afya nchini.
Mfuko wa Afya wa Pamoja umedumu kwa miaka 23 hadi
kufikia leo ambapo ni muunganiko wa pamoja baina ya Serikali
na Wadau wa Maendeleo kutoka Denmark, Korea, Ireland,
Switzerland, Canada, UNFPA, UNCEF na Benki ya Dunia
ambao huchangia katika huduma za afya nchini kwa kutoa fedha
na kuziweka kwenye akaunti moja na fedha hizo kutolewa moja
kwa moja kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini.



