Serikali kupitia Wizara ya Afya imeingiza ugonjwa wa Sikoseli katika
mpango mkakati wa kupambana na magonjwa yasiyoambukiza ili
kuweza kupambana nao na kuhakikisha huduma za vipimo na matibabu
zinapatikana katika vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya msingi.
Hayo yamesemwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Dkt. Seif
Shekalaghe kwa niaba ya Naibu Waziri Dkt. Godwin Mollel wakati wa
maadhimisho ya siku ya sikoseli duniani ambayo kitaifa yamefanyika
jijini Arusha.
Dkt. Shekalaghe amesema Serikali imeweka mikakati mbalimbali ya
kupambana na ugonjwa huo ikiwa ni pamoja na kuanzisha kliniki katika
Hospitali za wilaya, mikoa, Kanda na taifa hivyo wakati umefika kwa
wagonjwa kutosafiri umbali mrefu kutafuta huduma hizo.
Dkt. Shekalaghe ameongeza kuwa Tanzania ni nchi ya tano Duniani kwa
kuwa na idadi kubwa ya watu wenye Sikoseli ambapo kila mwaka
wanazaliwa watoto 11,000 na mpaka Sasa idadi ya watu wenye sikoseli
ni 200,000 ambapo watu 5 mpaka 7 kati ya 100 waliopo chini ya miaka
mitano hufa kwa sababu mbalimbali kutokana na madhara
yanayosababishwa na Sikoseli.
Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Arusha Dkt. Silvia
Mamkwe ameitaka jamii kuondoa mila potofu juu ya ugonjwa wa
Sikoseli badala yake wazingatie kufanya vipimo wakati wa kupata
wenza ili kuepuka kuoana wote wakiwa na vinasaba vya Sikoseli
vinavyofanana hali itakayosaidia kutozaa watoto wenye ugonjwa huo.
Mmoja wa mashujaa wa Sikoseli ambaye ameishi na ugonjwa huo kwa
miaka 44 Bi. Sanyu Singa amesema wao kama mashujaa wanakabiliwa
na changamoto nyingi lakini kubwa ni elimu juu ya Sikoseli
kutokuwepo katika jamii.