Rais wa Marekani Donald Trump amesema Venezuela itatoa mapipa milioni 30 hadi 50 ya mafuta kwa Marekani, kufuatia operesheni ya kijeshi iliyomuondoa Rais Nicolás Maduro madarakani.
Kupitia mtandao wake wa kijamii wa Truth Social, Trump alisema mafuta hayo yatakuwa ya ubora wa juu na yatauzwa kwa bei ya soko. Aliongeza kuwa mapato yatadhibitiwa na yeye binafsi kwa madhumuni ya kuwanufaisha wananchi wa Venezuela na Marekani.
Tamko hilo linakuja wakati Trump akidokeza kuwa sekta ya mafuta ya Marekani itaanza kufanya kazi nchini Venezuela ndani ya miezi 18, huku akitabiri uwekezaji mkubwa katika nchi hiyo. Hata hivyo, wachambuzi wanasema kurejesha uzalishaji wa mafuta wa Venezuela kwa viwango vya awali kunaweza kugharimu mabilioni ya dola na kuchukua hadi muongo mmoja.
Kauli ya Trump imetolewa siku moja baada ya Delcy Rodríguez kuapishwa kuwa rais wa mpito wa Venezuela. Rais wa zamani Nicolás Maduro yuko nchini Marekani akijibu mashtaka ya ulanguzi wa dawa za kulevya na umiliki haramu wa silaha.



